Mwenye kupaka midomo.
Nauliza si utani,wala sizuwi fitina
Naomba jibu wendani,lenye kina na maana
Hii rangi midomoni,huwa ina ma’na gani?
Mwenye kupaka midomo,hasa apigwaje kisi?
Mahaba mnatatiza,mabinti wa siku hizi
Nyoyo mnatuumiza,kisi sasa hatuwezi
Midomo mnashangaza,walahi mwatupa kazi
Mwenye kupaka midomo,hasa apigwaje kisi?
Rangi hii midomoni,nyengine hasa ni sumu
Haina raha jamani,mapenzi kukosa hamu
Mwatunyanyasa wendani,kisha na kutudhulumu
Mwenye kupaka midomo,hasa apigwaje kisi?
Majike mloolewa,lengo lenu huwa gani?
Kikweli mwajiumbuwa,hamvutii jamani
Na yule ulochumbiwa,kisi upigwaje hani?
Mwenye kupaka midomo,hasa apigwaje kisi?
Dume fulani majuzi,lilisaka sidechiki
Kapigwa kisi mjuzi,penzi na yake mikiki
Kurudi nyumbani mwizi,akajulikana haki!
Mwenye kupaka midomo,hasa apigwaje kisi?
Rangi zilitapakaa,midomo na lake shati
Ilivyozuka balaa,tafurani hatihati
Kisha mwisho wa fadhaa,ikachanwa ndoa cheti
Mwenye kupaka midomo,hasa apigwaje kisi?
Rangi zina ma’na gani,iwapo mnapendana
Mwalimu sasa sioni,wala situkui dhana
Mpunguzeni jamani,rangi haina maana
Mwenye kupaka midomo,hasa apigwaje kisi?
Sitaki kusema sana,hapa mwalimu nakoma
Nipeni jibu la ma’na,liridhishalo mtima
Nawangoja waungwana,naomba fanyeni hima
Mwenye kupaka midomo,hasa apigwaje kisi.
(Mwalimu Baxtone)